Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania ((Tanzania Forest Services (TFS) Agency))
ulianzishwa kisheria kupitia Tangazo la Gazeti la Serikali (GN 269) la tarehe 30/7/2010
na kuzinduliwa rasmi tarehe 18/7/2011. Kuanzishwa kwa Wakala wa Huduma za Misitu
ni kwa mujibu wa Sheria ya Wakala “the Executive Agencies Act Cap. 245 (Revised
Edition 2009)”, pamoja na Sera ya Misitu ya mwaka 1998, Sera ya Ufugaji Nyuki ya
mwaka 1998, Sheria za Misitu na Nyuki Sura 323 na Sura 224 za mwaka 2002.
Aidha, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania uliundwa kwa kuzingatia Programu ya
Serikali ya Maboresho katika Utumishi wa Umma ya mwaka 2000 (Public Service Reforms
Programme (PSRP 2000)). Programu hii ililenga kuimarisha Idara na Wakala (Ministerial
Departments & Agencies (MDAs)) katika kuhakikisha utoaji wa huduma bora na
madhubuti katika utumishi wa umma, ambapo Wakala zinakuwa na uwezo, motisha na
mbinu za mabadiliko yenye kuleta ufanisi na tija kiutendaji.
1.1 Lengo Kuu la Kuanzishwa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania
Kwa kuzingatia programu tajwa, Wakala wa Huduma za Misitu umeundwa kwa
madhumuni ya kuhakikisha: Uwepo wa usimamizi madhubuti na wenye ufanisi na tija wa
rasilimali za misitu na nyuki; kuongeza ubora na thamani ya kifedha katika kutoa huduma
kwa umma; na kuendelea kukuza na kuboresha uwezo wa kutoa huduma kwa umma.
Katika muktadha huu, masuala ya uendelezaji sera na sheria, pamoja na kanuni na taratibu
zake yanashughuliwa na Idara ya Misitu na Nyuki katika Wizara ya Maliasili na Utalii.
Hata hivyo majukumu ya Wakala yameongezeka licha ya kutoshughulikia sera na sheria.
Wakala umepanua wigo kibiashara na kuongeza maeneo ya uzalishaji miti na mazao ya
nyuki ili kukidhi mahitaji halisi, shughuli za uwekezaji, kuboresha njia mbadala za mapato
na uboreshaji wa hifadhi za misitu na nyuki kwa ujumla.
1.2 Dira
“Kuwa kielelezo bora katika usimamizi endelevu wa rasilimali za misitu na nyuki.”
1.3 Dhima
“Kuwa na usimamizi endelevu wa rasilimali za kitaifa za misitu na nyuki ili kuchangia
mahitaji ya kijamii, kiuchumi, ki-ikolojia na kiutamaduni kwa kizazi cha sasa na kijacho”.
1.4 Maadili makuu
Wakala wa Huduma za Misitu
Tanzania unaongozwa na maadili makuu kama
yanavyoainishwa hapa chini:
a. Uadilifu
b. Usiri/Kutunza siri
c. Kutoa huduma bora kwa wateja
d. Ubunifu na kuleta mabadiliko
e. Ufanisi na ufasaha
f. Kuzingatia weledi g. Uwazi na uwajibikaji
h. Kufanya kazi kwa ushirikiano
1.5 Majukumu Makuu
Majukumu makuu ya Wakala wa Huduma za Misitu ni pamoja na:
a. Kuanzisha na kusimamia Misitu ya hifadhi na Hifadhi za Nyuki za Serikali
kuu;
b. Kuanzisha na kusimamia mashamba ya miti (Picha Na.1) na manzuki za
Serikali kuu;
c. Kusimamia rasilimali za misitu na nyuki katika ardhi ya jumla (General Land);
d. Kusimamia utekelezaji wa Sheria za Misitu na Ufugaji Nyuki katika maeneo
yaliyo chini ya Wakala;
e. Kukusanya Maduhuli yatokanayo na mazao ya misitu;
f. Kutoa huduma za ugani katika maeneo ya Wakala;
g. Kufanya biashara ya mazao na huduma za Misitu na Ufugaji Nyuki;
h. Uperembaji na tathimini kuhusu utekelezaji wa kazi za Wakala.
Comments
Post a Comment